Tuesday, July 3, 2012

LEO NI MIAKA 20 TANGU KUTUNGWA KWA SHERIA YA KURUHUSU VYAMA VINGI; BADO UPINZANI NI SAWA NA UADUI!

Ndugu zangu, 
Tarehe kama ya leo miaka 20 iliyopita, yaani tarehe 2 Julai, 1992, Bunge la jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha sheria ya kuruhusu kuwepo kwa mfumo wa vyama vingi. 
Miaka 20 imetimu, tumepiga hatua, lakini, mpaka hii leo, bado upinzani kwa wengine unatafsiriwa kama ni uadui, na wakati mwingine ni uhaini. 
Na katika Tanzania yetu, wenye fikra za kukipinga Chama tawala, CCM na Serikali wamekuwa wakitengwa na hata kupewa majina mabaya. Nimeshawahi kumsikia mtu akiambiwa;
“Alaa, unaongea na Lipinzani hilo!” Kana kwamba aliyeitwa ‘ Lipinzani’ hakuwa Mtanzania na binadamu kama wengine.
Na hakika, katika kujadili hili la Katiba Mpya, tuna kila sababu ya kuipitia historia yetu. Maana, naamini, kuwa historia ni mwalimu mzuri. 
Itakumbukwa, katikati ya vuguvugu lile la mageuzi ya kisiasa miaka ya 90 mwanzoni, Watanzania zikatufikia habari; kuwa Oscar Kambona, aliyekosana na Nyerere na aliyekimbila uhamishoni Uingereza, alikuwa njiani kurudi nyumbani. Ujio wa Oscar Kambona ukawa gumzo la mjini na nje ya jiji. Kuna waliojiandaa kwenda uwanjani kumpokea.
Usiku mmoja ikasikika sauti ya Bw. Mrema redioni. Sauti ya Waziri wa Mambo ya Ndani. Mrema alitamka, kuwa kama Kambona angekanyaga mguu wake Dar es Salaam, basi, angekamatwa kujibu mashtaka ya uhaini.
Ni hofu ile ile ya Serikali hata wakati huo. Hofu ya kuimarika kwa fikra za upinzani na kukua kwa upinzani. Mrema akatumika au akajituma kuwatisha na kuwakatisha tamaa Watanzania. Kambona alikanyaga Dar, hakuwa na mashtaka ya kujibu. Ulikuwa ’ mkwara’ tu, kama wanavyosema mitaani.
Na Mrema, akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, aliifanya kweli kazi ya kuwa ’ Mbwa wa Serikali’. Alibwaka kweli kweli. Nakumbuka usiku mmoja mwanzoni mwa miaka ya tisini nilimsikia Mrema akiongea redioni kutishia maandamano ya CUF. Maandamano yale yalikuwa yahitimishwe kwa mkutano viwanja vya Mnazi Mmoja. Mwenyekiti wa CUF, Bw. James Mapalala ndiye alikuwa aongoze maandamano hayo na kuhutubia.
Augustino Lyatonga Mrema akaaunguruma redioni usiku ule. Alishusha ’ mkwara’ mzito. Kuwa maandamano hayo si halali na yangekutana na nguvu za dola. Kesho yake, CUF waliingia mitaani. Ndio, Ungangari wa CUF ulianza siku nyingi.
Pale Mnazi mmoja FFU wakamwagwa, na farasi wao pia. Virungu vilitembea. James Mapalala, Mwenyekiti wa CUF, hakuonekana. Kukawa na taarifa, kuwa anatafutwa na polisi.
Dar ilikuwa ndogo wakati huo, lakini James Mapalala hakupatikana .
Ninazo taarifa za kuaminika za Kibalozi, kuwa James Mapalala alikuwa amejificha kwenye moja ya makazi ya rafiki yake, balozi wa nchi moja ya Kimagharibi. Ni balozi gani huyo? Na nini hasa kilitokea miaka 20 iliyopita?
James Mapalala yungali hai. Huu ni wakati kwa waandishi vijana kuwatafuta wazee veterani wa harakati za mageuzi ya kisiasa hapa nchini. Wazee kama akina James Mapalala.
Hawa ni watu muhimu sana watakaotusaidia kupokea simulizi zao. Kisha ziwekwe kwenye maandishi, na iwe kumbukumbu za kihistoria. Ni historia yetu, tusiionee aibu. Ni urithi tutakaowaachia wajukuu zetu ili nao waweze kujifunza. Waweze kujitambua na kujenga mioyo ya uzalendo.
Na.Blogger Maggid Mjengwa.


No comments:

Post a Comment